Mali za Impala Hotel zauzwa Sh2.6 bilioni kulipa madeni

Mali za Impala Hotel zauzwa Sh2.6 bilioni kulipa madeni

Muktasari:

  •  Mali za Kampuni za hoteli maarufu za kitalii za Impala na Naura Spring Hotel zimeanza kuuzwa kwa amri ya mahakama ili kulipa zaidi ya Sh1.3 bilioni wanazodai wafanyakazi na wadeni wengine.

  


Arusha. Mali za Kampuni za hoteli maarufu za kitalii za Impala na Naura Spring Hotel zimeanza kuuzwa kwa amri ya mahakama ili kulipa zaidi ya Sh1.3 bilioni wanazodai wafanyakazi na wadeni wengine.

Mali hizo zinauzwa baada ya amri iliyotolewa na Msajili wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi Arusha, Ruth Masama.

Mahakama hiyo ilimuagiza dalali wa Kampuni ya Nutmeg Actioneers Property kuuza mali hizo kabla ya Oktoba 15, 2021.

Mali zilizouzwa ni pamoja na kiwanja kitalu  namba 16,17,18 19,20,21,22 na 23 vilivyopo eneo la Uzunguni jijini Arusha na kuwezesha kupatikana Sh2.65 bilioni ambapo wadai wengine ni pamoja na Benki ya NBC na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo ya udalali, Boniface Buberwa alimtangaza mshindi wa mnada huo kuwa ni Edmund Robert Koka ambaye ameweza kufikisha dau la thamani ya Sh2.65 bilioni lililoshindwa kufikiwa na washindani wengine tisa walioshiriki mnada huo.

"Mshindi wetu atapaswa kulipa asilimia 25 leo na baada ya siku 14 anatakiwa awe amelipa fedha yote na endapo atashindwa atapewa mshindi wa pili naye akishindwa atapewa mshindi wa tatu na yeye akishindwa mnada utarudiwa"amesema

Kwa upande wake mnunuzi wa Mali hizo Edmund Koka alishukuru kupata bahati hiyo kwani ushindani ulikuwa mkali na yeye ndio aliiibuka mshindi Kwa kutoa dau la sh 2.65 bilioni.