Mama aliyemchoma mikono mwanaye afungwa jela miaka mitano
Muktasari:
Mkazi wa Kijiji cha Shahende wilayani Geita, Mpipi Emanuel (33) amemhukumiwa kifungo cha miaka mitano jela kwa kosa la kumchoma mikono mwanaye Helena Bahati na kumsababishia maumivu.
Geita. Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita imemhukumu mkazi wa Kijiji cha Shahende wilayani Geita, Mpipi Emanuel (33) kifungo cha miaka mitano jela kwa kosa la kumjeruhi kwa kumchoma mikono, mwanaye Helena Bahati.
Hukumu hiyo katika kesi ya jinai namba 200 ya mwaka 2022 ilitolewa na hakimu mkazi wa mahakama hiyo, Samuel Maweda.
Amesema kitendo kilichofanywa na mwanamke huyo ni cha kikatili na kimesababisha ndoto ya Helena ya kuhitimu darasa la saba kutotimia
Awali mwendesha mashtaka wa Serikali, Shukrani Msuya aliieleza mahakama kuwa Oktoba 4, 2022 mshatakiwa alimpiga mtoto huyo na kumchoma moto mikono na kumsababishia maumivu kinyume na sheria.
Mshtakiwa alikiri kutenda kosa hilo na kuiomba mahakama imsamehe na kumpunguzia adhabu kwa kuwa ana familia ya watoto watano ambao wanamtegemea na kuwa hilo ni kosa lake la kwanza.
Maweda alisema kitendo kilichofanywa na mshtakiwa ni kinyume na sera ya nchi juu ya elimu kwa watoto wa kike.