Mamia wajitokeza alfajiri vituoni kupata chanjo Arusha

Muktasari:

  • Mamia ya watu wamejitokeza kupata chanjo ya corona katika jiji la Arusha na kuibua msongamano mkubwa wa watu.


Arusha. Mamia ya watu wamejitokeza kupata chanjo ya corona katika jiji la Arusha na kuibua msongamano mkubwa wa watu.

Watu hao wamejitokeza Kwa wingi katika vituo vya Levolosi na Kaloleni na baadhi wamefika alfajiri baada ya Jana kukosa chanjo.

Julius Laizer amesema jana alikwama kupata chanjo kutokana na kufika jioni bado watu wakiwa kituoni.

"Leo nimerudi mapema hapa Levolosi nadhani ntapata chanjo kwani mimi nipo sekta ya utalii ambayo tunahatari ya maambukizi," amesema.

Mary Mushi ambaye jana alipanga kupata chanjo kituo Cha Kaloleni alikwama pia kutokana na kufika usiku na kuahirishwa zoezi.

"Naimani leo nitapata chanjo ili niendelee na majukumu mengine," amesema.

Mkuu wa wilaya ya Arusha, Sophia Mjema amesema watu wa Arusha wamehamasika sana na chanjo na wamejitokeza Kwa wingi.

Naye Mkurugenzi wa jiji hilo, Dk John Pima amewataka wakazi wa Arusha kufika katika vituo vilivyotengwa na watapata chanjo.