Mkulima ajeruhiwa Hai, RPC aagiza uchunguzi wafugaji

Mifugo ikipita barabara Kware wilayani Hai mkoani Kilimanjaro

Muktasari:

  • Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro (RPC), Simon Maigwa amewaagiza viongozi wilayani Hai kuchunguza vibali kwa wafugaji walioingiza mifugo wilayani humo ili kufahamu uhalali kama walifuata sheria.

Hai. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro (RPC), Simon Maigwa amewaagiza viongozi wilayani Hai kuchunguza vibali kwa wafugaji walioingiza mifugo wilayani humo ili kufahamu uhalali kama walifuata sheria.

 Hatua hiyo imejiri baada ya mkulima wa Kijiji cha Mkombozi wilayani humo, Aranyieli Lema (80), kujeruhiwa vibaya kichwani na wafugaji ambao hawajulikani wanapotoka wakati akiwazuia wasiingize mifugo kwenye shamba lake.

Akizungumza na Mananchi jana Ijumaa, Agosti 6, 2022 Kamanda Maigwa amesema viongozi wa wilaya ni lazima kujua mifugo iliyupo katika maeneo yao imeingia kwa utaratibu unaotakiwa ili kuepuka vurugu kati ya wafugaji na wakulima.

"Ni kweli kwa sasa kwa hali ilivyo ya ukosefu wa malisho kwa ajili ya mifugo, wafugaji kutoka sehemu mbalimbali wamekuwa wakitembeza mifugo kwa ajili ya kutafuta malisho, hivyo lazima tujue kama mifugo inayofika katika maeneo yetu ina uhalila kuwepo hapo ili kuepusha ugovi,” amesema

Juzi, wakati wa mapokezi ya Mkuu mpya wa Mkoa huo, Nurdin Babu, Kamanda Maigwa alisema moja ya changamoto katika mkoa huo ni wingi wa mifugo iliyoingia katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo hivyo kuwataka viongozi kufanya tathimini na kutoa maamuzi yaliyo sahihi ili kuepusha migogoro.


“Kama nilivyokueleza kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ifiki kwenye kata ya Masama kusini Kijiji cha Mkombozi, kama wafugaji kuja kwao hapo kama walipewa vibali hali kwa ajili ya mifugo. Kwa majani ni shida lakini ni lazima wafuate utaratibu” amesema Kamanda Maigwa


Akizungumza na Mwananchi Digital akiwa nyumbani kwake, mkulima huyo Lema amesema siku ya tukio akiwa shambani kukata nyasi kwa ajili ya mifugo yake ng’ombe waliingia kwenye shamba lake na kuanza kuharibu mazao mbalimbali yakiwamo mbaazi na miti aliyopanda.

Amesema alipowauliza wafugaji sababu za kuingza mifugo yao kwenye shamba lake walianza kumshambulia kwa fimbo na kumjeruhi kichwani.