Mwanafunzi adumbukia kwenye dimbwi la maji, afariki
Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Kagera, Agustino Olomi
Muktasari:
Wanafunzi wengine wawili wa sekondari ya kata ya Kagoma walipigwa radi na kujeruhiwa.
Muleba. Mwanafunzi wa Shule ya Msingi Kahengele amefariki dunia baada ya kuanguka kwenye dimbwi la maji leo Agosti 24.
Dimbwi hilo limetokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika wilaya ya Muleba mkoani Kagera.
Pamoja na mwanafunzi huyo kuzama kwenye dimbwi, wanafunzi wengine wawili wa Shule ya Sekondari ya Kata Kagoma walijeruhiwa na radi na kukimbizwa katika hospitali ya Kagondo kwa matibabu.
Mwenyekiti wa kijiji cha Nsisha kata ya Kikuku wilayani Muleba Phagency Rwabuleza amemtaja mwanafunzi aliyefariki kwa kuzama kwenye dimbwi la maji kuwa ni Enock Judius (8) wa darasa la awali katika shule ya msingi Kahengele.
Rwabuleza amesema mwanafunzi huyo alianguka kwenye shimo hilo baada ya kuteleza akiwa na wenzake wakielekea nyumbani kwao kitongoji cha Kahengele wilayani Muleba.
"Hili ni tukio la pili katika kijiji changu watoto kuzama kwenye mashimo ya wazi yanayoachwa kwa kufyatua matofali na kuchimba changarawe," amesema Rwabuleza.
Kamanda wa jeshi la polisi mkoani Kagera, Agustino Olomi amethibitisha kutokea kwa kifo cha mwanafunzi huyo huku akiwataka wazazi na walimu kuwalinda watoto wao.