Mzumbe yapanga kuongeza wanafunzi

Muktasari:

  • Makamu mkuu wa chuo kikuu Mzumbe, Profesa Lugano Kusiluka amesema kuwa maboresho ya miundombinu yanayoendelea kufanywa na Serikali katika chuo hicho miaka michache ijayo kitakuwa na ongezeko la wanafunzi 10,000.

  


Morogoro. Makamu mkuu wa chuo kikuu Mzumbe, Profesa Lugano Kusiluka amesema kuwa maboresho ya miundombinu yanayoendelea kufanywa na Serikali katika chuo hicho miaka michache ijayo kitakuwa na ongezeko la wanafunzi 10,000.

Profesa Kusikuma amesema hayo leo wakati wa mahafali ya 20 ya chuo hicho yaliyohudhuriwa na mkuu wa chuo hicho ambaye pia ni Rais mstaafu wa Serikali ya mapinduzi Zanzibar, Dk Ally Mohamed Shein.

Amesema kuwa chuo hicho kimekuwa na utaratibu wa kuzungumza na waajiri ili kujua mahitaji ya soko la ajira na kuona namna ambayo wanaweza kuboresha mitaala hiyo ili iendane na soko hilo.

Akitoa salamu za chuo hicho mhadhili wa chuo hicho, Profesa Cyriacus Binamungu aliwataka wahitimu kutumia taaluma zao katika kutoa huduma kwa jamii kwa kuwa nchi bado ina mahitaji ya wataalamu mbalimbali wakiwemo wa Sheria.

Profesa Binamungu alitolea mfano wilaya ya Malinyi ambayo haina wakili hata mmoja wakati wilaya ya Ngara na Misenyi kukiwa na wakili mmoja.

Naye makamu mwenyekiti wa Baraza la chuo hicho, Prof Benadetta Killian amesema sekta ya elimu bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya mabadiliko ya teknolojia, mapinduzi ya nne ya viwanda na janga la Uviko 19.

Amesema kutokana na changamoto hizo taasisi za elimu zinapaswa kuchukua hatua za makusudi na za haraka kukabiliana nazo.