Takukuru yamrejesha mstaafu mamilioni aliyoporwa kwenye mikopo umiza

Muktasari:
- Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Mara imemrejeshea mwalimu mstaafu Sh30 milioni kati ya Sh66 milioni alizoporwa na mliyemkopesha Sh1.4 milioni.
Musoma. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Mara imemrejeshea mwalimu mstaafu Sh30 milioni kati ya Sh66 milioni alizoporwa na mliyemkopesha Sh1.4 milioni.
Akizungumza leo Jumatano Aprili 28, 2021 mkuu wa Takukuru Mkoa wa Mara, Hassan Mossi amesema fedha hizo zimerejeshwa baada ya ofisi yake kupata taarifa juu ya kuwepo wa mkopo huo aliodai ni kinyume cha sheria na taratibu za mikopo.
Amefafanua mwalimu huyo kutoka wilayani Rorya ambaye hakutaka kumtaja jina alikopa Sh1.4 milioni Januari 2018 na kwa mujibu wa makubaliano yao, alitakiwa kurejesha Sh3 milioni mara atakapopata mafao ya kustaafu.
Amebainisha kuwa Januari 2019 mafao ya mwalimu huyo yalitoka na mkopeshaji huyo ambaye hakutaka kumtaja jina alimlazimisha mstaafu huyo kumlipa Sh66 milioni baada ya kughushi mkataba wa mkopo.
"Baada ya kupata taarifa kuhusu jambo hilo tulifanya uchunguzi na hadi sasa mkopeshaji huyo amesharejesha Sh30 milioni, bado tunaendelea na uchunguzi ili aweze kurejesha fedha zote alizochukua kinyume cha makubaliano na taratibu zinazoongoza mikopo nchini" amesema Mossi.
Ameeleza kuwa wanaendelea na uchunguzi kuhusu suala hilo na kwamba walibaini mwalimu huyo alichukuliwa fedha zake na mtu aliyedai amemsaidia kulipwa mafao yake wakati kiuhalisia hakuna kazi aliyofanya.
Amesema mtu huyo alimtaka mwalimu huyo kumlipa Sh20 milioni fedha ambazo mwalimu huyo alimpa lakini baada ya Takukuru kuingilia kati jamaa huyo tayari amerejesha kiasi hicho chote cha fedha.