Uswisi, Tanzania zilivyojenga mizizi ya ushirikiano ndani ya miaka 40

Wanufaika la Mpango wa Uwezeshaji kwa Vijana (OYE), Jema Boniphace Mgomba (kushoto) na Agnes Lasimo (kulia) wakifunga paneli ya umeme jua (solar panel) kwenye paa la nyumba katika kijiji cha Pandambili, mkoani Moro

Muktasari:

  • Tanzania (zamani Tanganyika) inatimiza miaka 60 tangu ilipopata uhuru kutoka katika utawala wa Waingereza, Desemba 9, 1961, hatua inayoliwezesha Taifa hili kuandika historia mpya.

Tanzania (zamani Tanganyika) inatimiza miaka 60 tangu ilipopata uhuru kutoka katika utawala wa Waingereza, Desemba 9, 1961, hatua inayoliwezesha Taifa hili kuandika historia mpya.

Historia hiyo pamoja na mambo mengine inahusisha uhusiano, urafiki na ushirikiano kati ya Tanzania na mataifa mengine duniani.

Moja ya nchi ambazo zina uhusiano mzuri na Tanzania ni Uswisi. Hii ni nchi ambayo imekuwa ikishirikiana na Tanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi, kidiplomasia na kijamii.

Historia inaonyesha kuwa ushirikiano huo ulianza miaka mingi na shughuli za Uswisi zilikuwepo nchini Tanganyika baada ya kumalizika kwa Vita vya Kwanza vya Dunia wakati Waswisi walipoanza shughuli za kimisionari na kazi katika mashamba ya mkonge.

Kwa mfano, katika Wilaya ya Ifakara mkoani Morogoro, masista wa Baldegg (Baldegg Sisters) kutoka Uswisi walianzisha Zahanati mwaka 1927, ambayo baadaye ilibadilishwa na kuwa Hospitali ya St. Francis.

Hospitali hiyo imeendelea kuwepo hadi leo na imepandishwa hadhi na kuwa hospitali ya mkoa ikihudumia watu zaidi ya milioni moja katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara na wilaya za Kilombero, Ulanga na Malinyi mkoani Morogoro. Shughuli nyingine za maendeleo za Serikali ya Uswisi hapa nchini zilianza katikati ya miaka ya 1970 zikiwa zimejikita katika uboreshaji wa barabara za vijijini, afya na mafunzo ya kitaaluma.

Shughuli hizi zilikuwa zinasi-mamiwa na Shirika la Maendeleo na Ushirikiano la Uswisi (SDC) kupitia ofisi ya uratibu iliyopo Nairobi, Kenya.

Shughuli hizo zilisaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto za upatikanaji wa huduma za afya, kurahisisha shughuli za usafiri maeneo ya vijijini na kuwawezesha wananchi kupata mafunzo ya kitaaluma yaliyowasaidia kuajiriwa na kujiajiri.

Mwaka 1981 uhusiano kati ya mataifa hayo uliimarishwa zaidi na kuingia katika historia mpya baada ya kufunguliwa kwa ofisi ya ushirikiano kati ya Tanzania na Uswisi, iliyopo jijini Dar es Salaam.

Kufunguliwa kwa ofisi hiyo ilikuwa alama mpya ambayo iliifanya Tanzania kuwa moja ya nchi zilizopewa kipaumbele na Uswisi.

Mkuu wa Ofisi ya Ushirikiano nchini, Leo Nascher anasema mwaka 2021, ofisi ya ushirikiano kati ya Tanzania na Uswisi imeti-miza miaka 40 tangu ilipoanza kufanya shughuli zake hapa nchini.

"Katika kipindi cha miaka 40 ya uwepo wake, ofisi ya ushirikiano kati ya Tanzania na Uswisi imeleta mabadiliko makubwa katika jamii kutokana na jitihada zake za kuleta mabadiliko chanya," anasema Nascher.

Anasema moja kati ya jitihada ambazo zinafanywa na ofisi hiyo ni utekelezaji wa mipango ya kimaendeleo yenye lengo la kuondoa changamoto mbalimbali katika kimaisha."Mpango wa ushirikiano wa kimaendeleo wa miaka minne (2021-2024) kati ya Uswisi na Tanzania ni miongoni mwa juhudi za ofisi hiyo katika kuhakikisha ushirikiano kati ya mataifa hayo unaendelea kuimarika," anasema Nascher.

Ukienda sambamba na Ajenda ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDG’s) na mkakati wa ushirikiano wa kimataifa wa Uswisi wa mwaka 2021-2024, mpango huu ni mwendelezo wa juhudi za Uswisi katika dhamira yake ya kuiunga mkono Tanzania katika juhudi zake za kupunguza umaskini na kuwa jamii yenye usawa.

Hii ni moja ya programu za ushrikiano kati ya Tanzania na Uswisi, ambazo zimegusa maeneo muhimu ikiwemo uchumi na jamii.

"Lengo kuu la mpango huu ni kuwawezesha vijana, hasa wasichana, kuwa sehemu muhimu ya hitihada za nchi kujiletea maendeleo na malengo ya jumla ni kuwawezesha vijana hasa wa kike kujiendeleza kijamii na kiuchumi," anasema Nascher.

Lengo ni kuwawezesha vijana hao kuwa kichocheo kikubwa cha kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye usawa na kipato cha kati.

Mpango huu umejikita kwenye maeneo makuu matatu ambayo ni kuimarisha taasisi za Serikali, kulinda na kukuza haki za kutoa maoni na kuboresha afya na maisha ya vijana.

"Kupitia uimarishaji wa taas-isi za Serikali, Ubalozi wa Uswisi kupitia timu yake imara inayo chapa kazi imejidhatiti kuhakiki-sha inasaidia uimarishaji wa upatikanaji wa huduma bora za msingi kwa jamii," anasema Jacqueline Matoro, Ofisa Programu wa Ubalozi wa Uswisi Tanzania.

Anasema katika kutekele-za hilo, Ubalozi umekuwa ukishirikiana na Serikali katika kuzijengea uwezo taasisi zinazotoa huduma za afya kupitia misaada ya kiufundi pamoja na fedha ambazo hutolewa kupitia mfuko wa pamoja wa wadau wa kimaendeleo ili kusaidia mpango mkakati wa sekta ya afya.

Jacqueline anasema kuwa kutokana na kubadilishwa kwa utaratibu wa utoaji wa fedha za mfuko huo, kwa sasa fedha zinaelekezwa moja kwa moja kwenye taasisi za afya badala ya utaratibu wa awali zilipokuwa zinapelekwa Wizara ya Fedha kisha wizara hiyo kuzipeleka wilayani.

Chini ya utaratibu huo, Ubalozi unafanya kazi na taasisi zinazotoa huduma za afya kuzijengea uwezo na kutoa misaada ya kiufundi ili kuboresha huduma kupitia mabaraza ya afya ya wilaya.

Hivyo, kutoa mafunzo na kuwajengea uwezo watendeaji wa mabaraza ya afya ngazi ya wilaya ni miongoni mwa mambo muhimu katika eneo la kujenga uwezo wa taasisi za Serikali linalotekelezwa kwenye mpango huu.Katika ngazi ya kitaifa, Ubalozi umekuwa ukifanya mijadala kwa kushirikiana na wadau wake ili kusaidia kuchanganua maeneo ya kimkakati yanayotakiwa kufanyiwa kazi kabla ya kuanza utekelezaji.Vilevile, lipo eneo la kulinda na kukuza haki za kutoa maoni.

Uswisi, ikiwa na lengo la kuhakik-isha wananchi wana uhuru wa kujielezea, inafanya kazi na asasi za kiraia kuwapatia watu maeneo ya kutoa maoni yao ili yafike kwenye sehemu zinazohitajika kwa ajili ya kupatiwa ufumbuzi.

Suala hilo linatekelezwa kupitia asasi za kiraia ambazo zinafanya juhudi za kuandaa na kutengeneza majukwaa ya kutoa maoni kwa umma ili kuongeza ushiriki wa wanajamii kwenye masuala mbalimbali pamoja na kulinda haki za binadamu.

Kupitia mpango huu, wananchi wanapata nafasi ya kukutana na wafanya maamuzi, wanasiasa pamoja na viongozi, na kutoa maoni kwa yale wanayodhani yanatakiwa kufanyika katika mustakabali mzima wa kuleta maendeleo ya kweli.Ili wananchi waweze kushiri-ki katika kutoa maoni, ni lazima wapate taarifa sahihi.

 Hivyo, eneo hili pia linashirikisha vyombo mbalimbali vya habari ili kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi na kwa wakati ili kufahamu kinachoendelea kwenye nchi yao. Kupambana na rushwaRushwa inabaki kuwa kero kwa Watanzania. Ina athari katika maendeleo na inaathiri zaidi masikini.

Ili kukabiliana na kero hii, Uswisi inashirikiana na Taa-sisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Tanza-nia bara na Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi (ZAECA) Zanzibar, kutoa ushauri wa kitaalamu wa namna ya kuchunguza na kushtaki kwa ufanisi kesi tata za rushwa na kurejesha nchini fedha zilizoibiwa.

Uswisi inafahamu kwamba kuboresha afya na maisha ya vijana ni moja ya nguzo muhimu katika kuleta maendeleo ya kweli kwa kundi hilo na Taifa kwa ujumla.

Katika eneo hilo, Uswisi inalenga kuwezesha na kuboresha maisha ya vijana, hasa wa kike, kwa kuchangia katika kuongeza upatikanaji wa mafunzo ya ufundi stadi, ubunifu na afya ya uzazi.Kupitia programu yake ya Stadi za Ajira Tanzania (SET), Uswisi inasaidia kuboresha maendeleo ya mafunzo ya ufundi stadi (VSD) nchini Tanzania.

Programu ya SET, itakayotekelezwa na shirika la Swisscontact, inaendana na Mkakati wa Taifa wa Maendeleo ya Stadi za Ufundi (NSDS 2016-2026).

Mkakati huo unalenga kuimarisha uwezo wa kitaifa wa mfumo wa VSD na kukuza fursa za maendeleo ya stadi zinazotokana na mahitaji ya ajira. SET itaboresha matarajio ya ajira (kuajiriwa na kujiajiri) kwa kuchangia upatikanaji, umuhimu na ubora wa mafunzo ya ufundi stadi.

Uswisi pia inahamasisha huduma za umma na ushirikishwaji wa sekta binafsi ili kupanua wigo wa chaguzi kwa vijana. Hii itawawezesha kutafuta vyanzo vipya vya mapato na fursa za kuongeza tija za shughuli zao za kiuchumi.

Hii imesaidia kuwafikia vijana katika maeneo mbalimbali kupitia vikundi na kuwajengea uwezo wa kutambua na kutumia fursa zilizopo kujikwamua kiuchumi.

Uswisi imefanikiwa kuwafikia vijana na kuwapa elimu za masoko kwa kushirikiana na wachambuzi wa kimasoko ili kuhakikisha vijana wanapata taarifa sahihi za masoko na kupewa elimu ya ujasiriamali.

Haikuishia hapo, Uswisi, kupitia programu ya Opportunity for Youth Empowerment (OYE), inawasaidia vijana kujiajiri kwa kuanzisha miradi mbalimbali ya kilimo, ufugaji na ushonaji.

OYE ni miongoni mwa programu zilizobadilisha maisha ya vijana wengi katika maeneo mbalimbali nchini. Kutokana na uhusiano mzuri ulipo baina ya mataifa haya, katika miaka ijayo, Uswisi itaendelea kufanya kazi na washirika wa ndani ili kuwawezesha vijana, hasa wa kike, kujiendeleza kijamii na kiuchumi kupitia Mpango wa Ushirikiano wa Uswisi kwa Tanzania 2021–2024.

Kujua zaidi kuhusu programu ya maendeleo ya Uswisi nchini Tanzania, tembelea tovuti ya Ubalozi wa Uswisi: https://www.eda.admin.ch/daressalaam

 #SDC40TZ  #SwissEmbassyTZ