Waomba sheria ya watu wenye ulemavu mwaka 2004 ifanyiwe marekebisho

Arusha. Wadau kutoka sekta ya umma na binafsi wameshauriwa kuboresha huduma za afya kwa watu wenye ulemavu ikiwemo kujenga miundombinu ya kutosha katika vituo mbalimbali vya afya pamoja na  kuwepo kwa wataalamu wa kutosha katika kutoa huduma kwa watu wenye ulemavu hususani viziwi.

Hayo  yalisemwa  mkoani Arusha na mtoa mada katika mafunzo ya Shirika linalojihusisha na Maendeleo ya Vijana katika nyanja za Afya, Uchumi na Uongozi (DSW), Dk Fredrick Msigallah wakati akizungumza kwenye semina kuhusu afya ya uzazi kwa waandishi wa habari na maafisa habari iliyofanyika mkoani hapa na  kuandaliwa na Shirika la DSW.

Msigallah alisema sera ya watu wenye ulemavu ya mwaka 2004 imepitwa na wakati  hivyo inatakiwa ifanyiwe mapitio iendane na wakati kwa kuzingatia mkataba wa kimataifa wa watu wenye ulemavu wa mwaka 2006.
Alisema watu wenye ulemavu wamekuwa wakikabiliwa  na changamoto mbalimbali  katika kupata huduma jambo ambalo  huwakwamisha na wengi wao kuishia kukata tamaa.

"Tunaomba pia vyuo vya uuguzi viweke kozi za utoaji huduma kwa watu wenye ulemavu  ikiwemo mafunzo ya lugha ya alama iwe sehemu ya mitaala yao ili wataalamu wanaomaliza  wawe na ujuzi wa kutosha katika kutoa huduma kwa jamii ya watu wenye ulemavu hususani viziwi," alisema
Kwa upande wake Meneja Uraghibishi na Mahusiano kutoka DSW, Philomena Marijani alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwajengea uwezo wadau hao kuhusu afya ya uzazi katika jamii pamoja na huduma jumuishi ya afya na jinsia kwa watu wanaoishi na ulemavu.

Philomena alisema wamekuwa wakishiriki na kuangalia namna ya kuwasaidia watu wa makundi  maalumu katika kujikwamua  kiuchumi na kuweza kuondokana na changamoto mbalimbali.

"Kuna haja kubwa sana  ya kuwepo kwa wataalamu wa lugha za alama katika vituo vya afya ili kurahisisha huduma za afya kwa watu wenye ulemavu kwani wanakabiliwa na changamoto  nyingi sana wakati wa kufuata huduma hizo  na kushindwa kutatua changamoto zao kwa wakati," alisema.

Mmoja wa washiriki katika mafunzo hayo, Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Viziwi  na Jamii (DCPO), Ramadhani Hamisi alisema wamekuwa wakikabiliwa na changamoto kubwa katika kupata huduma za afya  kutokana na kutokuwepo kwa wataalamu wa lugha za alama hali ambayo inachangia  wengi wao kukosa huduma na kuendelea kuteseka.

"Kuwepo kwa wataalamu wa lugha za alama ndani ya hospitali kutasaidia  sana kwetu sisi kupata huduma rafiki na sahihi ndani ya jamii kwani wengi wa walemavu wamekuwa wakiendelea kuteseka kutokana na kukosekana kwa wataalamu hao hivyo naomba sana serikali itusaidie katika hilo," alisema