Nike yataja siri viatu vya pinki Kombe la Dunia
Mmoja wa viongozi wa Kampuni ya Nike, Odinga Nimako amefichua kwamba sababu ya uwepo wa idadi kubwa ya viatu vyenye rangi ya pinki katika Kombe la Dunia mwaka huu ni faida ya kisaikolojia inayowapa wachezaji.
Utafiti wa Nike ulionyesha kuwa wanamichezo hupendelea rangi kali na zenye kung'aa zaidi wanapokuwa katika mechi zenye uhitaji mkubwa wa matokeo ili kuongeza kujiamini kwao.
"Kile tunachosikia mara kwa mara kutoka kwa wateja na wanamichezo wetu ni kwamba unapovaa rangi kama pinki ambayo ni kali sana na inayoonekana kwa urahisi, ni kama unapaswa kuwa mchezaji mzuri sana ili kuivaa," alisema Nimako
Rangi hiyo inatajwa imefikia kiwango cha kukubalika kitamaduni duniani kote, jambo linaloifanya ivutie soko la watumiaji wa kawaida.
Mbali na hali ya kisaikolojia ya wachezaji, uchaguzi wa rangi ya pinki pia ulikuwa umefanyiwa utafiti makini ili kuwa na mwonekano mzuri zaidi katika matangazo ya kimataifa.
Wakati wa majaribio ya maendeleo ya bidhaa, Nike iligundua kwamba hakuna rangi iliyojitokeza zaidi dhidi ya rangi ya kijani ya nyasi kuliko pinki, jambo lililohakikisha mwonekano mzuri kwa mashabiki waliokuwa uwanjani na wale waliokuwa wakitazama kupitia luninga.
Inaonekana kwamba Adidas na Puma pia walifanya “ugunduzi” huo huo na kuamua kutumia pinki.
Hata hivyo, kwa kuwa karibu wachezaji wote sasa wanavaa pinki, chapa hizo zimefikia matokeo yaliyo kinyume kabisa na walivyotarajia — hakuna mchezaji wao anayejitokeza tena, isipokuwa wale wasiovaa pinki.