Soka waungana kupinga ukatili
Dar es Salaam. Timu za Simba, Azam na Singida Big Stars zimeungana kwa pamoja kupinga na kukemea ukatili wa wanawake na watoto kupitia kampeni ya 'Piga Mpira, Si Wanawake' iliyozinduliwa rasmi jana Dar es Salaam, chini ya usimamizi wa Shirika Lisilo la Kiserikali la Thamani Women Tanzania.
Akizungumza katika uzinduzi huo jana, Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamis Mwinjuma 'Mwana FA' kuwa mpira wa miguu ni mchezo namba moja nchini na una mashabiki wengi na kama wachezaji na viongozi watashiriki katika kampeni za kupinga ukatili kwa wanawake na watoto, jamii itabadilika na kuwa na fikra chanya.
“Ni wakati wa kutumia nafasi zetu kuunga mkono kampeni hizi ili jamii ibadilike, wachezaji na viongozi ni kioo cha jamii na wote tukiungana, tutafikia malengo yetu,” alisema Mwinjuma.
Mkurugenzi Kuu wa taasisi hiyo, Nafue Nyange alisema kuwa wameamua kutumia mpira wa miguu kwa lengo la kufikisha haraka ujumbe wao kwani mpira wa miguu kutokana na ukweli kuwa idadi kubwa ya wanaume wanapenda mchezo huo.
“Wachezaji wa timu hizo tatu watarekodi video na sauti ikipinga udhalilishaji na vitendo vya kikatili kwa wanawake na watoto. Kwa kuanzia tumechagua timu hizo tatu ambapo baadaye tutatanua wigo kwa kushirikisha timu nyingine.
“Nachukua fursa hii kuwapongeza viongozi wa timu hizi tatu na wadau kwa kutuunga mkono katika kampeni hii muhimu kwa ustawi wa jamii, tunaamini tutafanikiwa,” alisema Nyange.
Mtendaji Mkuu wa Simba, Imani Kajula alisema watatumia wachezaji wao na mitandao ya kijamii kupinga ukatili wa wanawake na watoto kwa nguvu zote.
Kauli hiyo iliungwa mkono na Ofisa Mtendaji Mkuu wa timu ya Azam FC, Abdulkarim Popat na wa Singida Fountain Gates FC, Olebile Sikwane.