Petroli, dizeli bei juu Zanzibar

New Content Item (1)

Muktasari:

Bei za mafuta ya petroli na dizeli zimekuwa zikipanda na kushuka kwa nyakati tofauti, jambo ambalo linaelezwa kusababishwa na mwenendo wa bei katika soko la dunia.

Unguja. Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (Zura), imetangaza bei mpya za mafuta ambapo za petroli na dizeli zimepanda wakati mafuta ya ndege yakishuka na taa yakiuzwa bei ya awali.

Hayo yamebainishwa leo Februari 8, 2024 na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa Zura, Mbaraka Hassan Haji wakati akizungumza na waandishi habari, ofisini kwake, Unguja.

Amesema, bei ya petroli kwa Januari ilikuwa lita moja Sh2,893, ambapo mwezi huu itauzwa kwa Sh2,933, likiwa ni ongezeko  kwa asilimia 1.38.

Haji amesema mafuta ya dizeli lita moja ni  Sh3,102 wakati mwezi uliopita yaliuzwa kwa Sh3,101, sawa na ongezeko la asilimia 0.03.

Pia, amesema lita moja ya mafuta ya taa ilikuwa inauzwa Sh3,200 na  mwezi huu yatauzwa bei hiyo hiyo.

Kwa upande wa mafuta ya ndege, lita moja iliuzwa Sh2,825 mwezi uliopita na mwezi huu yatauzwa Sh2,638 ikiwa imeshuka kwa  asilimia 6.69.

Mkurugenzi huyo amesema sababu za kuongezeka bei za petroli na dizeli ni kuongezeka kwa bei za mafuta hayo katika soko la dunia.

Hata hivyo, amesema mamlaka inawahimiza wananchi wote kununua mafuta katika vituo halali na kudai risiti za kielektroniki kila wanapofanya manunuzi.

Baadhi ya wananchi wametoa maoni yao kuhusiana na bei hizo akiwemo Ismail Abdalla anayesema wanaopanga wanapaswa kuzingatia hali ya wananchi, kwani wao ndio wanaoumizwa.

“Bei hizi za juu zinatuumiza sisi wananchi wa chini, maisha yetu ni magumu sana na tunahitaji mafuta hayo ili kuendesha shughuli zetu,” amesema Abdallah alipokuwa akizungumza na Mwananchi Digital.