Vigogo CCM watua Arusha na Lowassa

Muktasari:

Matson Chizii na Hamis Mjega ambao ni wanachama wa CCM wametua Arusha a na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa ambaye leo Jumamosi anarejea nyumbani kwake, Monduli mkoani Arusha


Arusha. Makada watiifu wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa aliohama nao CCM na kujiunga Chadema na sasa amerejea nao CCM, Matson Chizii na Hamis Mjega leo Jumamosi Machi 9, 2019 wametua pamoja na Lowassa uwanja mdogo wa Arusha.

Viongozi hao ambao wamewahi kushika nafasi kadhaa wakiwa CCM, walionekana wenye faraja baada ya kutua uwanjani Arusha saa 6:20 mchana.

Mgeja aliyewahi kuwa mwenyekiti wa CCM mkoa wa Shinyanga akizungumza na Mwananchi amesema wamerejea nyumbani CCM na wanatarajia wataendelea kutoa michango yao.

"Tumerudi nyumbani mimi na Lowassa ni marafiki na naimani tutaendelea kukijenga chama chetu CCM," amesema. Wengine ambao walitua ndege moja na Lowassa ni mke wa Lowassa, Regina Lowassa.

Baada ya kutua Arusha, Lowassa alipokewa na mjumbe wa NEC wa mkoa wa Arusha Daniel Awakii na kusalimiana na wana CCM na kwenda moja kwa moja chumba cha kupumzika wageni mashuhuri (VIP).