Mkuu wa Kanisa KKKT Askofu Shoo akemea ukanda, siasa na kulipa visasi

Muktasari:

Uongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) unakutana katika mkutano wa siku nne ulioanza jana Jumanne mkoani Arusha 

Arumeru. Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Fredrick Shoo amesema kanisa hilo linajivunia kazi ya utume ambayo wamekua wakiifanya tangu kuunganishwa kwa Dayosisi saba za makanisa ya kiinjili mwaka 1963 na sasa zimefikia 26 Tanzania.

Akizungumza katika ibada ya ufunguzi wa mkutano mkuu wa 20 jana jioni Jumanne Agosti 20,2019 katika Chuo Kikuu cha Tumaini Makumira Arusha nchini Tanzania, Askofu Shoo alisema mshikamano na maono ya viongozi wa kiroho waliotangulia wametoa mchango muhimu kufikia mafanikio hayo.

“Niwaombe viongozi na washarika kwa ujumla kuwa makini na mafundisho potofu kutoka kwa yeyote bali kudumu katika kweli ya Mungu na tusiwe watumwa wa ukanda na siasa bali tuwe imara kutenda lililo jema bila kulipa kisasi,” alisema  Askofu Shoo

Pia, alisisitiza amani na upendo katika kanisa hilo na jamii kwa ujumla.

Mkutano huo umewaleta pamoja wajumbe zaidi ya 250 nchini ambao pamoja na mambo mengi watamchagua Mkuu wa Kanisa hilo Ijumaa  hii ya Agosti 23,2019 atakayeliongoza kwa kipindi cha miaka minne ijayo.

Maaskofu wa Dayosisi 25 pamoja na wajumbe wengine wa mkutano huo tayari wapo katika Chuo Kikuu cha Tumaini Makumira kinachomilikiwa na kanisa hilo kuhudhuria mkutano huo isipokua Askofu mmoja wa Dayosisi ya Mbulu, Nicholaus Nsanganzelu ambaye ni mgonjwa.

Pia maaskofu wastaafu wanne ni miongoni mwa viongozi walioalikwa tayari wameshawasili ambao ni Levis Sanga na Hance Mwakabana wa dayosisi ya Kusini Kati (Makete),Paul Akyoo wa Dayosisi ya Meru  na Job Mbwilo wa dayosisi ya Kusini Magharibi(Matamba).

Endelea  kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi