Hizi hapa mbinu za kudhibiti ‘bando’

Hizi hapa mbinu za kudhibiti ‘bando’

Muktasari:

  • Suala la kurejea kwa vifurushi ni jambo ambalo linasubiriwa kwa hamu na wengi, ahadi nyingi zimetolewa mpaka sasa na watu wanaendelea kusubiri na tayari Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA) imeahidi kuwa jambo hilo litakamilika mapema.

Dar es Salaam. Suala la kurejea kwa vifurushi ni jambo ambalo linasubiriwa kwa hamu na wengi, ahadi nyingi zimetolewa mpaka sasa na watu wanaendelea kusubiri na tayari Mamlaka ya Mawasiliano nchini (TCRA) imeahidi kuwa jambo hilo litakamilika mapema.

Hata hivyo, ni muhimu watu kufahamu wanawezaje kupata huduma za intaneti kwa matumizi mahususi bila kutumia fedha nyingi.

Njia ya kwanza kudhibiti matumizi ya data ni kwenda kwenye mpangilio wa simu yako na kuzuia program ulizonazo zisifanye kazi isipokuwa unapozigusa. Unaweza kufanya hivi kwa kuangalia ni zipi zinatumia zaidi bando lako kupitia hukohuko kwenye mpangilio (Data usage settings).

Pia, mtumiaji wa simu anaweza kudhibiti matumizi yake kwa kuingia katika mpangilio wa simu au programu husika na kuzuia baadhi ya shughuli kutofanyika isipokuwa kwa idhini.

Kwa kuwa mtandao wa WhatsApp unatumiwa na wengi, mara nyingi mtu unaweza kudhibiti matumizi ya data kwa kutoruhusu mtandao huo kupakua kila kitu unachotumiwa. Unaweza kufanya hivyo kwa kuingia kwenye mpangilio wa WhatsApp, ukishafanya hivyo, picha, video na sauti hazitajipakua tena bila wewe kutaka.

Pia mtumiaji wa simu unaweza kuweka katika mpangilio wa simu kiwango cha matumizi ya data ambacho unataka kukitumia kwa siku na kiwango hicho kinapofikiwa, mfumo wa data hujizima yenyewe.

Tangu yalipotokea mabadiliko ya vifurushi, wananchi wamekuwa wakipaza sauti zao kutaka hali ya zamani na siku tano zilizopita Mkurugenzi TCRA, Dk Jabiri Bakari aliliambia gazeti hili kuwa suala la kurejesha vifurushi vya zamani litachukua chini ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 2.