‘Msiwatoze wananchi fedha wanapokuja kuchukua vitambulisho vya Taifa’

Mkuu wa Wilaya ya Lindi Shaibu Ndemanga alievaa suti nyeusi akimkabidhi mmoja wa Watendaji box la Vitambulisho vya Taifa. Picha na Bahati Mwatesa
Muktasari:
- Zaidi ya vitambulisho 4000 vitatolewa kwa wananchi wa Mkoa wa Lindi waliokuwa na namba za Nida.
Lindi. Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Shaibu Ndemanga amewataka watendaji wa vijiji, mitaa na Kata, kutoka katika Halmashauri ya Mtama na Manispaa ya Lindi kutowatoza wananchi gharama yoyote ya fedha pindi wanapokwenda kuchukua vitambulisho vyao vya Taifa.
Ndemanga ameyasema hayo leo Jumanne October 31, 2023 alipokuwa akikabidhi vitambulisho kwa watendaji wa vijiji na kata. Amesema kuwa wananchi wanapokwenda kuchukua vitambulisho vyao wasitozwe gharama yoyote kwani vitambulisho hivyo hutolewa bure.
"Niwaombe watendaji wote mliokuwa hapa mwananchi anapokuja kuchukua kitambulisho chake sitaki kusikia ametozwa fedha, kitambulisho cha Nida ni bure, pia ugawaji wa hivi vitambulisho ufanyike kwa siku saba,"amesema Ndemanga.
Akizungumzia ugawaji wa vitamvulisho hivyo, Ofisa Msajili wa vitambulisho vya Taifa mkoani Lindi, Oliver Mainya amesema kuwa jumla ya vitambulisho 426,741 vitatolewa kwa wananchi ambao tayari walikuwa na namba za Nida.
Naye Christina Kiwanga, Mtendaji wa Kata ya Mingoyo amesema vitambulisho vya Taifa vitasaidia hata kusafiri kwenda nchi nyingine.
“Mfano sisi ambao tupo huku karibu na Msumbiji, huwezi kubeba makaratasi mengi kupeleka sehemu husika, utachukua kitambulisho chako cha Nida taarifa zote watazipata,”amesema.