DC Moshi abwagwa uchaguzi CCM
Muktasari:
- Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Abbas Kayanda ameshindwa kung'ara kwenye uchaguzi wa CCM Wilaya ya Moshi vijijini katika nafasi ya Ujumbe wa mkutano mkuu Taifa baada ya wajumbe kumbwaga.
Moshi. Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Abbas Kayanda ameshindwa kung'ara kwenye uchaguzi wa CCM Wilaya ya Moshi vijijini katika nafasi ya Ujumbe wa mkutano mkuu Taifa baada ya wajumbe kumbwaga.
Uchaguzi huo wa Wilaya ambao ulimalizika jana Ijumaa Septemba 30, 2022 usiku, katika nafasi ya Mjumbe wa mkutano Mkuu wa CCM Taifa, mbali na Kayanda, pia walikuwepo wakuu wa wilaya watatu wa zamani, ambapo Raymond Mushi na Betty Machangu nao wameangukia pua, huku Regina Chonjo akichomoza kwa kuchaguliwa.
Msimamizi wa uchaguzi huo Ibrahim Mjanakheri amewatangaza wajumbe wa mkutano mkuu Taifa kutokea Moshi vijijini ambao wameshinda kuwa ni Leonard Waziri aliyepata kura 644, Regina Chonjo kura 587 na Prosper Tesha kura 517.
Amewataja wagombea walioshindwa uchaguzi huo na kura zao kwenye mabano kuwa ni Abas Kayanda (423), Betty Machangu (398), Ally Bady (323), Raymond Mushi (201), Brayton Shayo (68)na Ruwaichi Kaale (28).
Kwa nafasi ya mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Moshi Vijijini, msimamizi wa uchaguzi amemtangaza Cyril Mushi aliyekuwa akitetea nafasi hiyo, kushinda kwa kupata kura 919, dhidi ya Esther Kway aliyepata kura 29 na Abel Massawe kura 77.
Akizungumza baada ya kutangazwa mshindi, Mwenyekiti Mushi amesema tayari imepatikana timu ya ushindi katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka 2024 na uchaguzi mkuu 2025 na kiwataka wanachama wa chama hicho kuungana na kuwa wamoja ili kufanikisha hilo.
Aidha Mushi ameonya viongozi na wanachama wa chama hicho kutotumia mitandao ya kijamii kuchafua chama na kueleza kuwa hawatamvumilia wala kumfumbia macho mtu wa namna hiyo.
"Hatutamvumilia mtu yoyote ambaye atajaribu kuvuruga umoja wetu ndani ya chama, tutapambana naye. Wapo watu wanatuchafua kwenye mitandao, naomba niseme sitaruhusu shughuli za chama zifanyike kwenye mitandao, lazima kila mmoja ambaye ni mwanachama wa CCM aheshimu katiba ya chama,” amesema.