Msekwa: Uamuzi wa Chadema ni wa kikatiba
Muktasari:
Makamu mwenyekiti mstaafu wa CCM, Pius Msekwa amesema uamuzi wa kamati kuu ya Chadema kuwavua uanachama waliokuwa makada wake 19 kwa sababu ya kuapishwa kuwa wabunge wa viti maalum kinyume na ridhaa ya chama hicho ni wa kikatiba.
Dar es Salaam. Makamu mwenyekiti mstaafu wa CCM, Pius Msekwa amesema uamuzi wa kamati kuu ya Chadema kuwavua uanachama waliokuwa makada wake 19 kwa sababu ya kuapishwa kuwa wabunge wa viti maalum kinyume na ridhaa ya chama hicho ni wa kikatiba.
Spika huyo wa zamani wa Bunge amesema kwa uamuzi huo ni wazi kuwa wamepoteza sifa kuwa wabunge wa viti maalum kwa tiketi ya chama hicho.
Akizungumza na Mwananchi Digital leo Jumamosi Novemba 28, 2020 kuhusu uamuzi wa kamati kuu ya Chadema , Msekwa amesema katiba ya Tanzania inaagiza kwamba mbunge lazima awe mwanachama aliyependekezwa na chama fulani cha siasa, “inaeleza kuwa akikoma kuwa mwanachama wa chama kilichomleta bungeni na ubunge wake unakoma.”
“Ndiyo maana tunaona wanaohama kutoka chama kimoja kwenda kingine wanapoteza ubunge na uchaguzi mwingine lazima uitishwe, iwe ukiacha uanachama kwa kwenda chama kingine au ukifukuzwa na ubunge wako umekoma hayo ndiyo matakwa ya katiba,” amesema.
Amesema, “kwa msingi huo wabunge 19 waliofukuzwa siyo tena wabunge kwa sasa na itabidi chama kilichowapeleka bungeni kianze upya kupendekeza wanawake wengine watakaoshika nafasi hiyo.”