Wafanyabiashara 600 wamefunga biashara Geita

Muktasari:
- Wafanyabiashara zaidi ya 600 mkoani Geita wamefunga biashara zao mwaka 2020 kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kubadilisha maeneo ya kufanyia biashara.
Geita. Wafanyabiashara zaidi ya 600 mkoani Geita wamefunga biashara zao mwaka 2020 kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kubadilisha maeneo ya kufanyia biashara.
Hayo yamesemwa na meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Geita, Hashim Ngoda wakati wa semina ya uzinduzi wa programu maalum ya Serikali ya kukagua na kufuatilia matumizi sahihi ya mashine ya kieletroniki (EFD) .
Ngoda amesema wafanyabiashara kuhama maeneo yao na wengine kubadili biashara ni miongoni mwa sababu za kufungwa kwa bishara hizo.
Wakati meneja wa TRA akitaja sababu hizo mwenyekiti wa bodi ya wafanyabiashara eneo la mji mdogo wa Katoro, Deogratius Sangalali amesema wafanyabiashara wamefunga kutokana na kodi kubwa zinazotozwa na TRA na kusababisha watu kufilisika.
Amesema wafanyabiashara wanalazimika kuandika barua za kudanganya kuwa wamehama au kutoa sababu za ugonjwa kwa kuwa wakieleza kufilisika TRA hukataa kufunga biashara na kuwataka waendelee kufanya kuzifanya hata kama haziwalipi.