Wananchi wafunguka Lowassa kurejea CCM

Muktasari:

  • Wananchi wametoa maoni yao kwenye mitandao ya kijamii kuhusu uamuzi wa Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa kurudi CCM na kauli yake ya kutaka asiulizwe kwa nini amerudi kwenye chama chake cha zamani.

Dar es Salaam. Wananchi mbalimbali wametoa maoni tofauti kuhusu Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa kurudi CCM na kauli yake ya kutaka kutoulizwa sababu ya uamuzi wake huo ambao umewashangaza wengi.

Lowassa alihamia Chadema mwaka 2015 baada ya jina lake kukatwa wakati wa mchakato wa kutafuta mgombea urais wa chama hicho. Baada ya kukosa nafasi hiyo, Lowassa alihamia upinzani na kupewa nafasi ya kugombea urais akiwakilisha muungano wa vyama vinavyounda Ukawa.

Baadhi ya wananchi walioandika kwenye mitandao ya kijamii wamesema walitarajia angerudi kwenye chama chake, wengine wakisema alichelewa kufanya uamuzi huo na baadhi ya watu wakisema Chadema itaendelea bila yeye.

Respice Bimbiza ameandika kwenye ukurasa wa facebook wa Mwananchi kuhusu habari hii akisema “Sisi Chadema hatuna shida na wewe fisadi tena, kwanza ulichelewa kurudi kwenu CCM halafu hauna madhara yoyote kwetu Chadema, wewe ni gunia la misumari.”

Right Malila naye ameandika “Lowasa anaujua mziki wa Chadema, CCM amerudi kwa sababu ya...!”

Said Dodo anasema “hatuwezi kumuliza kwa sababu tunafahamu karudi kwa sababu ana udhaifu katika siasa na pia ana uroho wa madaraka.”

Daudi Msigwa anasema “umeona mali zako zinakamatwa na mkwe wako yuko ndani miaka miwili, huo ni uoga, mbona Sumaye wamechukua mashamba.”

Beatus Benedict ameandika “Duh, ukiwa CCM ni vituko tu, yaani unatupangia hata maswali ya kukuuliza!”