TTCL yaelemewa deni la Sh403 bilioni

TTCL yaelemewa deni la Sh403 bilioni

Muktasari:

  • Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imesema Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limelemewa na deni la Sh403 bilioni ilhali mtaji ilionao ni wa Sh243.

Dodoma. Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imesema Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) limelemewa na deni la Sh403 bilioni ilhali mtaji ilionao ni wa Sh243.

Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Japhet Hasunga amesema hayo jana Jumatano Oktoba 20, 2021 baada ya kuipitia ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2019/20 ambapo amesema wamebaini kuna viashiria katika Shirika hilo kutofanya vizuri kwakuwa lina mtaji hasi wa Sh132 bilioni na madeni makubwa kuliko mtaji wake.

“Hicho ni kiashiria kuwa bado shirika haliendi vizuri. Shirika letu linalipa hadi kodi lakini mapato yao hayajaingizwa katika vitabu vyao,” amesema Hasunga.

Alizitaja kampuni inayoshughulika na mkongo wa Taifa na kituo cha takwimu (data center) kwamba kamati imeona haja ya kukaa na Serikali ifafanue kwa nini mapato ya kampuni hizo hayaingizwi katika vitabu vya TTCL kama sheria inavyotaka.

Pia, amesema wamebaini soko la shirika hilo haijakaa sawa ukilinganisha na wapinzani wao wa kibiashara. Ili kulinusuru shirika hilo, Hasunga amesema Serikali inatakiwa kuongeza mtaji ama kuruhusu vyanzo vingine viingize mtaji huo.