VIDEO: Lugola asema laini zisizosajiliwa hazitazimwa

Muktasari:

Waziri wa Mambo ya Ndani nchini Tanzania,  Kangi Lugola amesema laini za simu ambazo hazitajasiliwa hadi kufikia Desemba 31, 2019 hazitazimwa.

Dodoma. Waziri wa Mambo ya Ndani nchini Tanzania,  Kangi Lugola amesema laini za simu ambazo hazitajasiliwa hadi kufikia Desemba 31, 2019 hazitazimwa.

Lugola ametoa kauli hiyo bungeni mjini Dodoma leo Jumatano  Novemba 13, 2019 katika kipindi ambacho sharti la kuweza kusajili laini ni kuwa na Kitambulisho cha Taifa ambacho upatikanaji wake ni mgumu na umekuwa kilio cha wengi.

Karibu katika maeneo mengi ya ofisi za Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) hufurika misururu ya watu kuanzia alfajiri na mapema wakitaka japo wapate namba tu waweze kwenda kusajili laini zao za simu kabla ya Desemba 31 siku ambayo laini zote zisizosajiliwa zitazimwa.

Lugola ameyasema hao wakati akijibu mwongozo wa  mbunge wa Kavuu (CCM) Dk Pudensiana Kikwembe.

Dk Kikwembe amesema upatikanaji wa vitambulisho hivyo umekuwa mgumu huku akitolea mfano hali ilivyo jimboni kwake.

“Uandikishaji umekuwa shida na kama tunavyojua mwisho ni Desemba. Naomba kauli ya Serikali ili waweze kupata vitambulisho” amehoji.

Katika majibu yake Lugola amewatoa hofu Watanzania kuwa utambuzi, usajili na utoaji wa vitambulisho kwa wananchi wenye sifa ni endelevu.

SOMA ZAIDI

Amesema Watanzania wasiwe na wasiwasi hilo ni zoezi endelevu na ndio maana kila mwaka kuna Watanzania wanaofikisha miaka 18.

“Hili la kusajili laini kwa kutumia vidole kwamba lazima uwe na kitambulisho cha Taifa ndio lina mwisho.”

“Lakini naomba niwatoe wasiwasi Watanzania wote kwamba maelekezo ya Rais Magufuli hakuna Mtanzania ambaye simu yake itazuiwa kutumika eti kwa sababu hana kitambulisho cha Taifa na laini yake haijasajiliwa,” amesema Lugola.

SOMA ZAIDI

Amesema lengo la usajili na utambuzi ilikuwa kwa watu milioni 23.3 lakini hadi sasa wamesajili Watanzania milioni 20.5, “hadi sasa tumezalisha namba za vitambulisho kwa Watanzania milioni 15.5.”