Shahidi kesi ya kina Mbowe ashindwa kumtambua mshtakiwa

Muktasari:

Ofisa Uchaguzi manispaa ya Kinondoni, Victoria Wihenge ameshindwa kumtambua mtuhumiwa wa kesi ya uchochezi inayowakabili viongozi tisa wa chama kikuu cha upinzani  nchini Tanzania cha Chadema akiwemo mwenyekiti wake, Freeman Mbowe.


Dar es Salaam. Ofisa Uchaguzi manispaa ya Kinondoni, Victoria Wihenge ameshindwa kumtambua mtuhumiwa wa kesi ya uchochezi inayowakabili viongozi tisa wa chama kikuu cha upinzani  nchini Tanzania cha Chadema akiwemo mwenyekiti wake, Freeman Mbowe.

Amesema mtuhumiwa huyo, Esther Matiko ambaye ni mbunge wa Tarime Mjini alikwenda ofisi ya mkurugenzi wa manispaa ya Kinondoni kudai kiapo kwa ajili ya kusimamia uchaguzi.

Wihenge ameshindwa kumtambua mshtakiwa huyo leo Alhamisi Agosti 22, 2019 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakati akitoa ushahidi.

Mbowe na viongozi wengine wanane wa chama hicho wakiwemo wabunge sita wanakabiliwa na kesi ya jinai namba 112/2018 yenye mashtaka 13 yakiwemo ya uchochezi.

Wihenge ambaye ni shahidi wa saba katika kesi hiyo, ametoa ushahidi wake mbele ya hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo, Thomas Simba.

Akiongozwa na wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon, shahidi huyo amedai Februari 16, 2018 walifika viongozi wawili wa Chadema katika ofisi hizo kudai viapo vya mawakala wa kusimamia uchaguzi.

Shahidi huyo aliwataja viongozi hao waliofika katika ofisi hizo kuwa ni mbunge wa viti  maalumu wa Chadema,  Suzan Lyimo na  Matiko.

"Walipofika katika ofisi yangu walijitambulisha majina yao na wanatoka Chadema na kusema wamekuja  kufuatilia viapo vya mawakala wao kwa ajili ya kusimamia uchaguzi uliokuwa unatarajia kufanyika Februari 17, 2018.”

"Niliwaambia kiapo cha kutunza siri si kiapo kwa ajili ya kutambulisha mawakala, bali mawakala wanatakiwa wapewe barua ya utambulisho inayoandikwa kutoka kwa msimamizi wa uchaguzi kwenda kwa msimamizi wa kituo cha kupiga kura, ambapo mawakala wa vyama husika hukuta majina yao katika vituo vya kupiga kura.”

Shahidi huyo licha ya kuwataka viongozi hao waliofika katika ofisi yake alishindwa kumtambua mshtakiwa Matiko ambaye yupo katika chumba cha mahakama.

Alipoulizwa kama anaweza kumtambua mmoja wa washtakiwa ambaye alifika katika ofisi yake kwa ajili ya kudai kiapo, alidai kuwa hamkumbuki kwa sababu  Februari 16, 2018 alipomuona hadi sasa ni muda mrefu, hivyo hawezi kumkumbuka.

Hata hivyo, kabla ya shahidi huyo kuendelea kutoa ushahidi kuliibuka mabishano yaliyotaka kuzuia vurugu baina  ya mawakili wa Serikali na wale wa upande wa utetezi.

Mmoja wa mawakili wa utetezi, Hekima Mwasipo alinyanyuka katika benchi na kwenda kuchungulia sehemu aliyokaa shahidi bila ruhusa ya mahakama.

Mwasipu alidai kuwa alikuwa wanataka kujiridhisha kama shahidi hajashika simu au kipande cha karatasi wakati akitoa ushahidi.

Hakimu Simba alimuonya Mwasipu na kumtaka kutoa taarifa kama anaona shahidi huyo ameshika kitu na sio kunyanyuka kienyeji bila ruhusa ya mahakama.

Mbali na Mbowe, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni wabunge; Esther Matiko (Tarime Mjini);  Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini); Halima Mdee (Kawe), John Heche (Tarime Vijijini), Ester Bulaya (Bunda Mjini), John Mnyika (Kibamba).

Wengine katibu mkuu wa chama hicho, Dk Vicent Mashinji na naibu katibu mkuu  (Zanzibar), Salum Mwalimu

 

Endelea kufuatilia Mwananchi kupata kinachojiri mahakamani hapo