Serikali yapunguza tozo kwa asilimia 30

Serikali yapunguza tozo kwa asilimia 30

Muktasari:

  • Serikali imepunguza viwango vya tozo mpya ya Serikali kwa asilimia 30 na viwango vilivyopunguzwa vitatangazwa rasmi kwa tangazo la Serikali Septemba Mosi 2021.

Dar es Salaam. Serikali imepunguza viwango vya tozo mpya ya Serikali kwa asilimia 30 na viwango vilivyopunguzwa vitatangazwa rasmi kwa Tangazo la Serikali Septemba Mosi 2021.

Uamuzi huo unafuatiwa na malalamiko ya wananchi na watoa huduma za miamala yaliyoibuka mara baada ya kuanza kwa tozo hizo Julai 15 mwaka huu baada ya bajeti mpya iliyopitishwa na Bunge ikiwa na tozo hizo mpya kuanzai Julai Mosi.

Taarifa iliyotolewa na Wizara ya Fedha na Mipango leo Agosti 31,2021 imerejea kauli ya Rais Samia Suluhu ya Julai 19, 2021 aliyewaelekeza mawaziri wa Fedha na Mipango na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kupitia upya tozo za miamala ya simu baada ya kusikia kilio cha wananchi kuhusu tozo hizo.

“Katika kutekeleza maelekezo hayo, leo wametia saini marekebisho ya Kanuni za Tozo za Miamala ya Kieletroniki za Kutuma na Kutoa Fedha za Mwaka 2021,” imeeleza taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imeongeza kuwa Serikali imefanya majadiliano na watoa huduma za simu ambao nao wameridhia kupunguza viwango vya tozo wanazotoza katika miamala ya kutuma na kutoa fedha kati ya mtandao na mtandao mwingine kwa asilimia 10.

“Serikali inaamini kuwa uamuzi huo utatoa nafuu kwa wananchi na kuiwezesha Serikali kupata fedha za kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo kama ilivyokusudiwa wakati tozo hizo ziliporidhiwa na kupitishwa na Bunge la Bajeti la Mwaka 2021/2022.”